Kitaifa

Gazeti makini

Philipo Mulugo

Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi

Ripoti ya Ushindani ya Dunia ya mwaka 2013 – 2014

Ripoti hiyo inaonyesha kwamba, Tanzania inashika nafasi ya 125 duniani kwa kuwa na taasisi zinazovutia mazingira ya kiushindani kibiashara miongoni mwa mataifa 128, jambo ambalo ni mporomoko wa hatua tatu kutoka nafasi ya 120 katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita iliposhika nafasi ya 120

Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe

Kwa mujibu wa Mbowe, Operesheni Kimbunga halikuwa na maandalizi ya kutosha na lilifanyika kwa chuki na uonevu

Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli

Dk. Magufuli: Tatizo la kuharibika kwa barabara linasababishwa na ujenzi duni wa wakandarasi, lakini kwa kiasi kikubwa huharibiwa na magari yanayozidisha mizigo.

Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia

Mmoja wa viongozi wanaounda ushirika huo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha NCCR-Mageuzi, James Mbatia alithibitisha taarifa hizo huku akisisitiza kuwa nia ya kufanya hivyo ni kuhakikisha wanaiondoa madarakani CCM mwaka 2015.

Sunday, November 10, 2013

Zitto: Nimechoka Kuzushiwa na kuchafuliwa

Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, Zitto Kabwe
Na Agatha Charles, Tabora
NAIBU Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Zitto Kabwe, ameibuka na kutoa kauli na tamko dhidi ya tuhuma mpya dhidi yake zilizosambazwa katika mitandao ya intaneti katika siku za hivi karibuni.

Zitto, ambaye pia ni Naibu Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni na Mbunge wa Kigoma Mjini, amefanya hivyo akitumia majukwaa mawili tofauti.

Mwanasiasa huyo kijana ambaye amejipambanua kuwa mtetezi wa misingi ya utaifa, raslimali za nchi, uchumi na masuala ya utawala bora ndani na nje ya chama chake, alifanya hivyo kwa mara ya kwanza juzi jioni, wakati alipokuwa akihutubia mkutano mkubwa wa hadhara katika uwanja wa Kolimba wilayani Kariua, Mkoa wa Tabora.

“Katika umri huu mdogo, nimepigwa mishale mingi ya kisiasa, mimi ni binadamu nina damu, nikipigwa hii mishale damu inatoka, ninaumia, sasa nimechoka kupigwa mishale, lazima sasa tuambiane ukweli,” alisema Zitto.

Saa kadhaa baada ya hotuba yake hiyo, Zitto ambaye kwa muda mrefu sasa amekuwa katika mzozo wa wazi na baadhi ya viongozi wenzake ndani ya Chadema, alisambaza tamko la maandishi ambalo lilibeba ujumbe unaofanana na ule alioutoa Kariua.

Awali katika mkutano wa Kariua, Zitto alisema alikuwa hayuko tayari kuendelea kukaa kimya pasipo kuchukua hatua zikiwamo za kisheria wakati akichafuliwa.

Alisema alikuwa ameshamwandikia barua Katibu Mkuu wake, Dk. Wilibrod Slaa, akihoji iwapo taarifa ya kumchafua iliyosambazwa katika mitandao ya intaneti chini ya kiichwa cha habari kisemacho “Taarifa ya Siri ya Chadema” ni ya chama hicho au la.

Zitto aliyekuwa akizungumzia matokeo ya ziara yake ya kufuatilia kuhusu fedha zilizofichwa na baadhi ya Watanzania katika mabenki ya Uswisi na kwingineko Ulaya, alieleza kusikitishwa na kile alichodai kuwa ni kikundi cha watu ndani ya Chadema ambacho kimekuwa mstari wa mbele kumpaka matope.

“Wakati nafanya kazi hii ya hatari ya kufuatilia hizo fedha zilizofichwa nje ya nchi, navunjwa nguvu na watu ambao tuko chama kimoja kwani imekuwa ni kawaida unapofanya siasa, lazima upate mashambulizi na sasa nashambuliwa na chama changu.

“Katika hali ya kawaida, wenzagu tulionao katika chama ndio waliopaswa kunipa nguvu, kwani tuna kazi kubwa ya kupambana na ‘lidude likubwa linaloitwa CCM,” alisema Zitto.

Akifafanua na pasipo kutaja jina la mtu, alisema kuna watu wachache ambao hawana kazi ndani ya chama hicho ambao shughuli yao imekuwa ni kugonganisha viongozi ili wagombane.

Akirejea historia ya kuchafuliwa kwake, Zitto alisema hali hiyo ilianza mwaka 2009 baada ya kujitokeza na kugombea uenyekiti wa taifa wa Chadema akichuana na Freeman Mbowe.

Alieleza kushangazwa na hali hiyo ambayo alisema inakinzana na kile kilichotokea mwaka 1995 wakati waasisi wawili wa Chadema, Edwin Mtei na Bob Makani walipojitokeza kusaka uteuzi wa mtu ambaye angekiwasilisha chama hicho katika kugombea urais.

Alisema mara baada ya mmoja wao kupitishwa na chama chao, makundi yote yaliyotokana na harakati hizo yalivunjwa na chama kikaendelea kubakia kimoja.

“Mwaka 2009, niliamua kugombea uenyekiti kwa sababu nilijua katika chama chetu kuna demokrasia inayomruhusu kila mmoja kugombea nafasi anayoona inamfaa. Lakini, kitendo cha mimi kugombea kikaonekana ni nongwa japokuwa wapo wengine waliogombea mwaka 1998 na hakukuwa na migogoro.

“Sasa, watu wanaona uchaguzi (ndani ya Chadema) unakaribia, vurugu na ugomvi vinaanza bila sababu yoyote. Lakini, kwa mtu kama mimi niliyeingia kwenye siasa nikiwa mdogo, najua tumefanya mengi na tumeibua mambo mengi pia,” alisema akijigamba.

Katika taarifa yake ya maandishi aliyoisambaza jana, Zitto aligusia kwa muhtasari kuhusu tuhuma kadha wa kadha ambazo ndizo zilizosababisha aandike barua kwa Dk. Slaa.

“Nilipokuwa katika ziara ya Bara la Ulaya kati ya Oktoba 21 mpaka Novemba 2 mwaka huu, nilipokea kwa njia ya barua pepe ripoti inayoitwa Taarifa ya siri ya Chadema ambayo pia ilikuwa imesambazwa katika mitandao ya kijamii.

“Taarifa ya Chadema inasema Chadema kimekuwa kikichunguza mwenendo wangu tangu mwaka 2008 hadi 2010 na kubaini kuwa mimi napokea fedha kutoka CCM ili kuivuruga Chadema.

“Ripoti hiyo ilinihusisha pia na mwananchi raia wa Ujerumani, Andrea Cordes, ambaye kwa mujibu wa ripoti hiyo, alinisaidia kupokea na kuhifadhi kiasi cha dola za Marekani 250,000 kupitia kwenye akaunti yake binafsi,” alisema Zitto.

Katika tamko lake hilo, Zitto aliita taarifa hiyo iliyojaa mambo mengi ya kimaadili, kuwa ni ya “kutunga na iliyojaa uongo wa kiwango cha kutisha”

Mbali ya hilo, Zitto alieleza kusikitishwa, kukasirishwa na kufedheheshwa na taarifa hiyo ambayo alisema ilikuwa ikilenga kumtoa katika nia yake ya kutaka Watanzania wafaidike na utajiri wao.

Kutokana na hali hiyo, Zitto alisema hawezi kukubali watu watumie jina lake na uanasiasa wake kumchafua yeye na watu wengine wasiohusika kwa sababu ya kutaka kutimiza malengo yao ya kidhalimu.

Zitto katika taarifa yake hiyo alisema tayari raia wa Kijerumani aliyedaiwa kumfichia fedha alikuwa amekana tuhuma hizo kupitia maelezo alyoyatoa kwa viongozi wa Chadema.

Kama hiyo haitoshi, Zitto alieleza kukerwa pia na hatua ya ripoti hiyo kulitaja jina la Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dk. Charles Kimei ikimhusisha na yeye kuficha fedha zinazomhusu yeye.

 “Niseme mapema, kwamba tangu kuzaliwa kwangu, sijawahi hata mara moja kukutana na Dk. Kimei popote pale ndani au nje ya nchi. Kumuingiza mtu ambaye amejenga jina lake kwenye taaluma ya kibenki kwa sababu tu ya lengo ovu la kumchafua Zitto Zuberi Kabwe si uungwana bali ni unyama,” alieleza mwanasiasa huyo.

Akiendelea, Zitto alisema alikuwa amepokea taarifa za kutishiwa maisha na mtu aliyemtaja kwa jina la Theo Mutahaba ambaye pamoja na mambo mengine alimtaka aache kupambana na masuala ya ufisadi.

“Kwa maana hiyo, natarajia kuchukua hatua kali za kisheria dhidi ya wote ambao wamehusika na utungaji na uenezi wa taarifa hii, nitahakikisha wahusika wanatafutwa na kufunguliwa mashitaka stahiki ya upotoshaji na kuchafuana.

“Nimeamua kujitolea maisha yangu kwa ajili ya Watanzania na kama alivyopata kusema Rais mstaafu wa Afrika Kusini, Nelson Mandela, “Struggle is my life,” alihitimisha Zitto taarifa yake hiyo.

Kenya yamuunga mkono JK

Rais Jakaya Kikwete
Na Benjamin Masese, Dar es Salaam
WAZIRI wa Mambo ya Nje wa Kenya, Amina Mohamed, ameipongeza Tanzania kwa hatua ya kutangaza kuwa haiko tayari kutoka katika Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), kama ilivyodhaniwa hapo awali.

Akizungumza Dar es Salaam jana, alisema Kenya inaunga mkono hotuba ya Rais Jakaya Kikwete aliyoitoa Novemba 7, mwaka huu kuwa haitajitoa na wala haitakuwa chanzo cha kuvunjika kwa EAC.

Alisema bila Tanzania hakuna Afrika Mashariki na bila Afrika Mashariki hakuna Tanzania.

“Kama unavyojua Kenya na Tanzania tumekuwa tukiijenga Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa muda mrefu, tuko na mafanikio mengi, kuna mambo mengi tumeyafanya, kuna njia ndefu imebakia na kuna mambo mengi yasiyoweza kupimwa kati ya nchi hizi.

“Tuna tumaini kwamba tutaendelea kuijenga Afrika Mashariki kwa nguvu zote na tutawasiliana na watu wetu kwa sababu tunataka watu wetu waishi vema na wawe majirani wazuri na tuendelee kuwa hivyo,” alisema Amina.

Amina ambaye ametumwa na Rais Uhuru Kenyata kuja kutoa ujumbe huo, alisema ni vyema nchi hizo zikaendelea kushirikiana kwa kuwa zenyewe ni za kwanza kuunda umoja huo, hivyo ziendelee kuungana kwa ajili ya kuudumisha.

Alisema walikuwa na wasiwasi kuwa Tanzania ingejitoa kutoka EAC, kutokana na hali iliyojitokeza kwa baadhi ya nchi kuendesha mikutano yao bila kuishirikisha pamoja na Burundi.

Alisema kuwa hakuna namna ambavyo Tanzania na Kenya zitatenganishwa kwa namna ambavyo zimejenga muingiliano mkubwa wa kijamii na kiuchumi, huku akiomba Tanzania kuisaidia kusukuma ombi la Kenya la kutaka kesi inayomkabili Rais Kenyatta iahirishwe kwa mwaka mmoja zaidi kwa ajili ya kumpa fursa ya kutekeleza majukumu yake ya kitaifa.

Kwa upande wake, Waziri wa Mambo ya Nje wa Tanzania, Bernard Membe, alisema Serikali yake imefurahi kuona Kenya imekuwa nchi ya kwanza kuipongeza kwa kuinusuru EAC kama ilivyokuwa mwanzoni na kujenga jumuiya ya watu na si ya viongozi.

Aliahidi kushirikiana na Kenya katika masuala mbalimbali likiwamo la kutaka kesi inayomkabili Rais Kenyatta katika mahakama ya ICC iahirishwe kwa mwaka mmoja zaidi.

Katika hatua nyingine, Chama cha Wananchi (CUF) kimesema kamwe ushirikiano wa Kenya, Uganda na Rwanda wa kuzitenga Tanzania na Burundi katika mipango ya EAC usingedumu kwa sababu uongozi wao ni wa kidikteta.

Akizungumza Dar es Salaam jana juu ya hotuba ya Rais Kikwete kuhusu EAC, alisema chama hicho kinaunga mkono msimamo wa Tanzania.

Alisema CUF kinalaani vikali vitimbwi vilivyokuwa vikifanywa na Rais wa Rwanda, Kenya na Uganda na kuitenga Tanzania na Burundi na kuongeza kuna haja sasa ya kuwa na tahadhari na viongozi hao katika suala la usalama wa raia na nchi kwa ujumla.

Alisema ushirika wa nchi hizo na mipango yao iliyokuwa ikifanyika isingedumu, kwa sababu uongozi wa Uganda na Rwanda ni wa kidikteta huku Kenya haina umoja wa kitaifa kutokana na kugawanyika vipande viwili.

“Ninachomuomba Rais Kikwete watakapokutana wakuu wa nchi hizo awape vidonge vyao, najua mwezi huu Baraza la Mawaziri litawasilisha mapendekezo ya majadiliano ya mkutano wa 15 kwa wakuu wa nchi,” alisema na kuongeza:

“Tumesikia baada ya hotuba ya Rais Kikwete, wameanza kujing’atang’ata lakini walichokuwa wakifikiria kukifanya ni ndoto za mchana, mfano Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta tangu achaguliwe anasuasua kufanya mikutano upande wa upinzani wake na hilo limeifanya nchi kukosa umoja wa kitaifa.

“Rais Yoweri Museveni wa Uganda amekuwa mstari wa mbele kuharakisha kufikia Shirikisho la Kisiasa kwa lengo la kutaka kuwa Rais wa kwanza wa Shirikisho la Afrika Mashariki.

“Shirikisho la kisiasa la Kenya, Uganda na Rwanda hizo ni ndoto na wanajifurahisha katika karne hii ya 21, shirikisho lazima lijikite katika mfumo wa demokrasia, Kenya imepiga hatua kubwa kujenga demokrasia lakini haijafanikiwa kujenga umoja wa kitaifa.

“Namuomba Rais Kikwete kuwa makini katika suala la soko la pamoja hasa katika ajira, ardhi na uhamiaji hivyo vitu visiingizwe katika soko la Afrika Mashariki bila kutafakari, Watanzania bado wamezubaa katika ardhi yao.

“Kuna jambo limejificha katika EAC, mimi nadhani ziara ya Rais Barack Obama kuja Tanzania ilielekea kutowafurahisha, ndio maana Kenya ilifikia hatua ya kususia mkutano wa wafanyabiashara wa Afrika ulioandaliwa na Corporate Council on Africa.

“Pia uhusiano kati ya Tanzania na Rwanda umezorota baada ya Rais Kikwete kuwapa ushauri viongozi wenzake katika mkutano wa Umoja wa Afrika kwamba njia pekee ya kumaliza migogoro ya kisiasa na kuleta amani katika nchi za Kongo, Rwanda na Uganda ni kufanya mazungumzo mezani.

“Jambo jingine ni baada ya Tanzania kukubali kupeleka wanajeshi wake Kongo kama sehemu ya Jeshi la Umoja wa Mataifa kuleta amani mashariki ya Kongo, ambapo limesaidia kusambaratisha kundi la waasi wa M23.”

Lowassa: Nasikitishwa elimu duni shule za kata

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa
WAZIRI Mkuu mstaafu na Mbunge wa Monduli (CCM), Edward Lowassa, amesikitishwa na kiwango duni cha elimu katika shule za sekondari za kata na baadhi ya vyuo vya elimu ya juu.

Akizungumza katika harambee ya kuchangia mfuko wa elimu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Usharika wa Kijitonyama, alisema kiwango cha elimu katika shule hizo kinamsikitisha kwa kuwa ni cha chini.

“Napenda niseme wazi kuwa kiwango cha elimu katika shule za kata na baadhi ya vyuo vikuu, kwa kweli ni vya chini, hili mimi linanisikitisha sana kwa sababu elimu bora ni mkombozi kwa mtoto wa Kitanzania,” alisema Lowassa.

Alipongeza kanisa kwa kusaidia juhudi za Serikali katika kuimarisha na kuboresha elimu, ambapo shule nyingi za kanisa zimekuwa na kiwango cha juu cha elimu.

Alitumia nafasi hiyo kuonyesha misuli yake kisiasa na kijamii ambayo ni marafiki wanaomsindikiza katika harambee mbalimbali.

“Sasa napenda Watanzania kupitia kwenu kuwaonyesha hawa marafiki zangu ambao wamekuwa wananisindikiza katika harambee, maana kumekuwa na maneno maneno,” alisema Lowassa baada ya wakili maarufu, Sadock Magai kuwasilisha michango ya marafiki.

Marafiki wa Lowassa walichangia Sh milioni 50 ambao ni Lawrence Masha, Innocent Macha, Bashir Awale, Hamis Kindoroko na Lemmy Bathelemew.

Aidha, Naibu Waziri wa Kazi na Ajira, Dk. Makongoro Mahanga, alichangia Sh milioni tatu na Mbunge wa Kinondoni (CCM), Idd Azan, alichangia Sh milioni mbili.

“Nampongeza na kumshukuru Idd Azan kwa kuja kwake kunisindikiza na kuchangia, hii ndiyo Tanzania ninayoijua, isiyo na dini, watu wa dini zote mnashirikiana,” alisema Lowassa.

Katika harambee hiyo, jumla ya Sh milioni 615 zikiwa ni fedha taslimu pamoja na ahadi zilipatikana na kuvuka lengo ambalo lilikuwa ni Sh milioni 250.

Tuesday, November 5, 2013

Taswira ya Tanzania kiuwekezaji yadorora

Taswira ya Tanzania kiuwekezaji yadorora
*Rushwa, miundombinu, umeme vyaiponza
*Yashika nafasi ya 145 kati ya mataifa 189
*Nyota ya Rwanda yang’ara kimataif
a

Na Gabriel Mushi
TASWIRA ya Tanzania katika ubora wa mazingira ya kiuwekezaji na kwa kuwa na fursa zinazovutia biashara kimataifa imeendelea kuporomoka, Rai Jumatano limebaini.

Ripoti mbili za kimataifa zilizotolewa na taasisi mbili za kiuchumi na kibiashara zinazoheshimika, Benki ya Dunia na ile ya Kongamano la Biashara la Dunia zote zinatoa taswira hiyo ya mdororo ambao umewashtua baadhi ya wadadisi wa masuala ya uchumi na uwekezaji.

Dodoso la kwanza linaloiweka Tanzania katika sura hiyo ya mporomoko limo katika ripoti ya ‘The Global Competitiveness Report 2013–2014 (Ripoti ya Ushindani ya Dunia ya mwaka 2013 – 2014).

Ripoti hiyo inaonyesha kwamba, Tanzania inashika nafasi ya 125 duniani kwa kuwa na taasisi zinazovutia mazingira ya kiushindani kibiashara miongoni mwa mataifa 128, jambo ambalo ni mporomoko wa hatua tatu kutoka nafasi ya 120 katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita iliposhika nafasi ya 120.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo inaeleza kwamba, mporomoko huo unachangiwa kwa kiwango kikubwa na kuzorota kwa mambo katika maeneo kadhaa yakiwamo yale ya taratibu za kisheria na kimaadili.

Ripoti hiyo inaainisha kwamba katika kipindi hicho cha mwaka mmoja, kumekuwa na kushamiri kwa vitendo vya rushwa kulinganisha na miaka iliyopita sambamba na kudorora kwa uwazi katika masuala yanayohusu uandaaji wa sera.

Mbali ya hayo, miongoni mwa mambo yanayotajwa kuathiri taswira ya ushindani wa Tanzania kibiashara ni ubovu au uhafifu wa miundombinu kama barabara, kukosekana kwa umeme wa uhakika na huduma zisizoridhisha za bandari.

“Kwa upande mwingine miundombinu ya Tanzania bado ni duni huku huduma za barabara na bandari zikiwa hafifu na kukosekana kwa uhakika kwa nishati ya umeme,” ilisema ripoti hiyo.

Ripoti hiyo inaonyesha Tanzania inashika nafasi ya 106 kwa kuwa na matendo mengi ya rushwa, ya 134 kwa kuwa na miundombinu duni na nafasi ya 131 kwa kukosekana kwa umeme wa uhakika.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, ingawa Tanzania inaonekana kuwa na idadi kubwa ya wanafunzi wanaojiunga na elimu yua msingi inatajwa kuwa miongoni mwa mataifa yenye idadi ndogo zaidi duniani kwa wanafunzi wanaojiunga na elimu ya sekondani na vyuo vikuu.

Kwa mujibu wa viwango vilivyoainishwa katika ripoti hiyo, Tanzania inatajwa kuwa ni nchi ya 134 kwa kuwa na idadi ya wanafunzi wanaojiunga na sekondari huku ikishika nafasi ya 138 kwa wale wanaopata elimu ya vyuo vikuu.

Kama hiyo haitoshi, ripoti hiyo pia inaitaja Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zenye fursa duni kwa upande wa maendeleo ya teknolojia ya kompyuta (Tehama) na ya simu za mikononi ikiwa nafasi ya 126 miongoni mwa mataifa 148.

Kwa upande wa Ripoti ya Benki ya Dunia (Doing Business Report 2014) imeonesha kuwa Tanzania imeendelea kuporomoka kwa nafasi tisa kutoka nafasi ya 136 mwaka 2012 hadi nafasi ya 145 mwaka huu kwa kuwa na mazingira mepesi yanayovutia biashara.

Uchambuzi wa ripoti hiyo inaonyesha kwamba, kabla ya kufikia hatua hiyo mwaka huu, miaka miwili tu iliyopita (2011) Tanzania ilikuwa ikishika nafasi ya 128 kabla ya kuporomoka zaidi kwa nafasi nane katika kipindi cha mwaka mmoja tu na baadaye kwa nafasi 19.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo iliyojumuisha nchi 189 ulimwenguni na kuwekwa hadharani Oktoba 29, mwaka huu, taifa dogo la Rwanda linaonekana kuwa kinara kwa kushika nafasi ya kwanza Afrika Mashariki na miongoni mwa mataifa yenye uchumi mdogo duniani.

Katika ripoti hiyo pia Tanzania imetajwa kutawaliwa na vitendo vya rushwa na urasimu katika maeneo ya upatikanaji wa huduma muhimu, ambazo kwenye nchi nyingine zinapatikana kwa urahisi.

Maeneo yaliyoanishwa na ripoti hiyo ni kama vile upatikanaji wa kibali cha ujenzi wa nyumba ( nafasi ya 177 kati ya nchi 189), hati ya kumiliki nyumba (nafasi ya 146 kati ya nchi 189) na usumbufu kwenye ulipaji wa kodi (nafasi ya 177 kati ya nchi 189).

Katika maeneo mengine, ripoti hiyo inaonyesha kwa upande wa ugumu wa kupata mikopo (nafasi ya 130 kati ya nchi 189), ugumu wa kusajili na kupata leseni ya biashara (nafasi ya 119 kati ya nchi 189), na ugumu wa kupata nishati ya umeme (nafasi ya 102 kati ya nchi 189).

Akizungumzia ripoti hiyo mwanasiasa na mchumi wa kimataifa, Profesa Ibrahimu Lipumba, alisema hali hiyo inajitokeza kutokana na kukosekana kwa utashi wa kisiasa na uongozi wenye dira madhubuti ya kufanya biashara na kuongeza ajira.

Profesa Lipumba alieleza kukubaliana na ripoti zote hizo mbili ambazo zimetolewa na Benki ya Dunia na taasisi isiyokuwa ya kiserikali ya World Economic Forum (WEF).

“Tanzania iko chini sana katika ushindani wa kiuchumi kwa sababu asasi zake za kiuchumi ni dhaifu na hazifanyi kazi kwa ufanisi, rushwa na ufisadi unazidi kuongezeka, na maumuzi ya sera hayako wazi na siyo thabiti.

“Mameneja wa kampuni kubwa zinazofanya biashara Tanzania wameeleza kuwa matatizo makubwa ya shughuli za kiuchumi Tanzania ni pamoja na ukosefu wa mikopo, rushwa na ufisadi, miundombinu mibovu, utendaji mbovu na urasimu wa watumishi wa serikali na mfumko wa bei,” alisema.

Alifafanua kuwa ili kupima ushindani wa kiuchumi wa kila nchi, watafiti wamechunguza mambo ya msingi yanayochochea ukuaji wa uchumi na uletaji wa maendeleo kwa ujumla.

Alisema ili Tanzania iweze kushindana na kunufaika katika ulimwengu wa utandawazi inahitaji iwekeze katika miundombinu ya barabara, reli, bandari, viwanja vya ndege, ufuaji na usambazaji wa umeme, miundombinu ya maji safi na maji taka TEHAMA na kuboresha elimu ya msingi, sekondari na vyuo vikuu.

Kwa upande wake Mhadhiri Mwandamizi kutoka Chuo Kikuu cha Mzumbe, Dk. Honesty Ngowi, alisema hilo ni pigo kwa serikali kwa sababu juhudi zinazooneshwa na serikali katika kuvutia uwekezaji nchini zimegonga mwamba.

“Suala la rushwa, na urasimu ndio chanzo cha haya yote kwa sabahu tunaona kuwa tangu mwaka 1960 hadi miaka ya 1980, serikali ilikuwa ikijipanga kuweka mikakati mbalimbali ya kuvutia wawekezaji, lakini cha ajabu hadi kufikia sasa ndio kwanza tunazidi kushuka.

“Tunatakiwa kujitathmini tumekosea wapi, na namna gani ya kuondokana na matatizo haya kwani hata katika awamu hii suala la kuvutia wawekezaji limekuwa likipigiwa debe sana, lakini hakuna kitu tunazidi kushuka,” alisema

Anguko hilo la Tanzania kiuchumi limekuja katika kipindi ambacho serikali ya awamu ya nne iko katika mikakati kadhaa ya kuboresha mazingira ya uwekezaji ili kuwavutia wawekezaji nchini.s

Benki ya Dunia imekuwa na taratibu za kutoa ripoti ya mazingira ya kufanya biashara katika nchi zote duniani kila mwaka.

Wakati Tanzania ikiporomoka kwa nafasi tisa nchi jirani ya Rwanda iliyokuwa na hali ngumu ya kufanya biashara, imefanikiwa kurekebisha mazingira ya biashara na kushika nafasi 32 kati ya nchi 189.

Ikumbukwe kuwa mwaka jana Rwanda ilikuwa ya 54 kwa hali hiyo nchi hiyo inayoongozwa na Rais Paul Kagame imepanda juu kwa nafasi 22.

Nchi zinazoongoza kwa ushindani wa kiuchumi wa mataifa ni Uswissi, ikifuatiwa na Singapore, Finland, Ujerumani, Marekani, Swiden, Hongkong, Uholanzi (Netherlands), Japan na Uingereza

Katika nchi za Afrika, inayoongoza kwa ushindani wa kiuchumi ni Mauritius inayoshika namba ya 45, ikifuatiwa na Afrika Kusini ambayo ni ya 53 na ya tatu ni Rwanda iliyoshika nafasi ya 66 katika orodha ya nchi 148.

Mauritius imeipiku Afrika Kusini iliyokuwa inaongoza mwaka jana.

Elimu ya Tanzania imekosa mkombozi

Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philipo Mulugo
NA ELIZABETH HOMBO
NIMEKUWA nikitatizwa na mfumo wa elimu nchini, ingawa nami ni mmoja wa watu waliopitia kwenye mfumo huo, lakini ukweli ni kwamba umekuwa hauna tija kwa wananchi.

Mfumo wa elimu na sekta ya elimu kwa ujumla imetawaliwa na matatizo. Waathirika wakubwa kwenye suala hilo ni Mtanzania fukara mwenye kipato kisichoeleweka.

Kukosa kwake uwezo wa kumsomesha mtoto wake kwenye shule za gharama, kunamfanya kuendelea kukubaliana na uduni wa elimu nchini.

Matatizo kwenye elimu yamekithiri zaidi kwa walimu ambao hawathaminiwi.

Tumeshuhudia migomo mbalimbali ya walimu ambao wamekuwa wakidai haki na maslahi yao.

Hata hivyo migomo yao imekuwa ikizimwa kwa amri ya Mahakama Kitengo cha Kazi, wanalazimishwa kurejea kazini, jambo hilo linawafanya kuingiwa na ganzi ya kutekeleza majukumu yao kikamilifu.

Ni jambo gumu kwa mtu kukubali kuwajibika kikamilifu wakati hali yake kifedha si nzuri.

Mara kwa mara walimu wamekuwa wakigoma kufundisha kutokana na kutolipwa madai yao ya msingi.

Hata hivyo mara kadhaa Serikali imekuwa ikiahidi kutekeleza madai ya walimu.

Madai ya msingi ya walimu ni mengi, mathalani Serikali iliombwa kulipa madai hayo kwa asilimia 100, lakini ikashindwa na baadaye kuomba ilipe kwa asilimia 67. Hata hivyo Serikali haikufikia asilimia hizo na badala yake imekomea asilimia 24, hatua hiyo inawaweka walimu kwenye hali ngumu ya maisha na mwelekeo wa elimu nchini.

Kutokana na hilo, hakuna ubishi kwamba walimu wengi wanafundisha kwa mtindo wa bora liende, hawafundishi kwa moyo kama inavyotakiwa, wanafanya hivyo kwa sababu mioyo yao imetawaliwa na masononeko.

Pamoja na walimu kuwa na madai lukuki kama hayo, bado Serikali imekuwa ikija na mipango hafifu kwa kudai kuboresha mfumo wa elimu jambo ambalo halifanyiki.

Hata yale mabadiliko yanayofanyika hayawashirikishi kikamilifu wahusika ambao ni walimu.

Mabadiliko hayo yamekuwa yakifanywa na wanasiasa ambao mara nyingi wamekuwa wakiyaangalia matakwa yao ya kisiasa na si matakwa ya sekta husika.

Wanasiasa wamekuwa wakiweka mbele maslahi yao binafsi badala ya majukumu waliyopewa.

Wanashindwa kuwashirikisha wataalamu ambao wanafahamu nini cha kufanya ili kuwasaidia wananchi kuondokana na elimu duni.

Yapo masuala ya ajabu yanayofanywa na wanasiasa kama yale ya kubadili viwango vya matokeo.

Pengine haya yanatokea kwa sababu viongozi wakuu wa wizara pamoja na kuwa na taaluma ya ualimu, lakini wametawaliwa na siasa.

Kwa maana hiyo ni lazima watekeleze matakwa yao ya kisiasa kabla ya kugeukia matakwa ya nchi.

Hilo linasababisha kushuka kwa viwango vya ufaulu kila mwaka.

Tazama mchezo wa kisiasa ulivyokosa haya, walianza kwa kufuta matokeo ya mitihani ya kidato cha nne mwaka jana, kisha wakatangaza matokeo mapya ambayo hayakuwa na nafuu yoyote.

Uamuzi huo ulifanywa kisiasa zaidi haukuwa na chembe ya utaalamu na utafiti juu ya kile wanachokifanya.

Baada ya tukio hilo sasa wamekuja tena na jipya kwa kubadilisha madaraja eti wamefuta daraja sifuri na anayepata daraja hilo atakuwa amefaulu kwa wastani wa daraja la tano, hata kama atakuwa amepata alama F kwenye masomo yote.

Ni wazi kwamba, hatua hii itazidisha kuzalisha wanafunzi mbumbumbu na bila shaka litakuwa ni taifa la ajabu kuwahi kutokea duniani.

Bado napata shida, inakuwaje mtu aliyepata sifuri aonekane amefaulu? Hawaoni kwa kufanya hivyo wanazidi kuwafanya wanafunzi wawe wavivu kusoma na kuendekeza mambo ya anasa badala ya kuzingatia masomo?

Kwa hali hiyo ni wazi wanafunzi wengi watapunguza moyo wa kujituma katika masomo yao kwa sababu wanajua hakuna kufeli kama ilivyokuwa awali, ambapo walijitahidi kusoma ili wasipate sifuri.

Hivi kweli katika maamuzi haya Serikali huwa inawashirikisha wadau wa elimu? Kutokana na haya ndio maana nahoji nani atakuja kuinusuru elimu ya Tanzania au ndio elimu yetu imekosa mkombozi? Je, tutegemee mkombozi kutoka nchi nyingine wakati jukumu hilo liko kwenye uwezo wetu.

Katika hali inayosikitisha Serikali inatangaza uamuzi huo huku matokeo ya mwaka jana yakionesha wanafunzi wakiandika majina ya wachezaji kama Lionel Messi na wengine wakichora michoro ya Zombi.

Katika muktadha huu Serikali inapoamua kuwabeba wanafunzi na kutangaza ufaulu mpya, unaleta maswali kuwa labda lengo la elimu yetu ni kujaribu kupata ufaulu badala ya kuikomboa nchi.

Kuanzia utawala wa Rais Mwinyi tuliona aliyekuwa Waziri wa Elimu, Jackson Makwetta akipendekeza mambo mbalimbali ambayo yangewezesha kuibadili elimu yetu.

Lakini kuanzia wakati huo tumezidi kushuhudia tume zilizoundwa pasipokuwa na majibu ya maana, kwani badala ya kuikomboa jamii zimekuwa zikijifurahisha na kuweka kabatini ripoti zote.

Kujiuzulu ni uadilifu wa kukiri upungufu

MTU anapokubali nafasi ya uongozi, maana yake ni kwamba anakubali kubeba wajibu mzima kuhusiana na ufanisi wa majukumu yake mahali pale anapopaongoza.

Kwa bahati mbaya sana, viongozi wetu nchini ni wepesi wa kupokea sifa kutokana na utendaji mzuri wa wale walio chini yao. Lakini mambo yanapokwenda vibaya, viongozi hao hao ndio huwa wa kwanza kujiweka mbali na makosa yaliyotendeka.

Tunasema kuwa kimsingi “kujiuzulu” si sawa na “kukiri kosa” moja kwa moja kwamba umelitenda.

 Kinyume chake, kujiuzulu ni tabia ya uadilifu, ambapo mhusika anakiri upungufu wake katika kusimamia majukumu yake.

Katika nchi zilizoendelea, ambazo tunapenda kuiga mienendo yao, kujiuzulu ni dhana ya uungwana na uadilifu. Viongozi hujiuzulu kazi zao inapodaiwa au wanapojihisi wao wenyewe kuwa wameshindwa kusimamia majukumu yao kama inavyopasa.

Aidha, hujiuzulu wao wenyewe bila shinikizo kutoka mahali popote baada ya kuzingirwa na kashfa, ama wao binafsi kama wao au sehemu wanazoziongoza kushindwa kuonyesha ufanisi na matarajio ya wale waliowapa dhamana.

Kwa Tanzania, hili jambo limekuwa gumu mno kwa viongozi kulielewa. Hawataki kujiuzulu hata mahali ambapo makosa yao yanaonekana dhahiri!

Rais mstaafu wa Awamu ya Pili, Ali Hassan Mwinyi, aliwahi kujiuzulu akiwa waziri baada ya Wizara ya Mambo ya Ndani aliyokuwa akiiongoza kukumbwa na kashfa, lakini uamuzi wake huo haukumzuia kuwa Rais.

Huko nyuma wananchi, wakiwamo baadhi ya viongozi na wabunge, mara kadhaa walimtaka aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini wakati huo, William Ngeleja, kujiuzulu kwa kushindwa kufikia matarajio ya Watanzania ya kuwapatia umeme wa uhakika.

Yeye aliwajibu kuwa hatajiuzulu ng’o, na kweli hakujiuzulu hadi mabadiliko ya Baraza la Mawaziri yalipofanyika.

Ngeleja hayuko peke yake. Yumo aliyekuwa Waziri wa Fedha, Mustafa Mkullo, aliyekuwa Waziri wa Maliasili na Utalii, Ezekiel Maige, aliyekuwa Waziri wa Uchukuzi, Omar Nundu, aliyekuwa Waziri wa Viwanda na Biashara, Cyril Chami na aliyekuwa Waziri wa Nchi katika Ofisi ya Waziri Mkuu akisimamia Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), George Mkuchika.

Wapo wengine, wakiwamo wakuu wa taasisi, ambao walitajwa na wamekuwa wakiendelea kutajwa katika ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), kwamba wanahusika katika kufanya ubadhirifu wa fedha za umma.

Huu ndio utamaduni wa viongozi wa Kitanzania, kwa maana kwamba kiongozi hatoki madarakani hadi apigwe mawe.

Hivi karibuni baada ya matokeo mabaya ya mtihani wa kidato cha nne, ambayo yalisababisha baadhi ya wanafunzi kujiua, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa, naye kwa jeuri kubwa aliwaambia Watanzania kuwa hatajiuzulu.

Kisa? Eti kwani akijiuzulu kitendo hicho kitaboresha elimu nchini! Maneno yake hayo ya kujiamini, aliyasema bila woga wala aibu.

Wiki iliyopita mjini Dodoma, wabunge walichachamaa wakiwataka wabunge watano, akiwamo Waziri Mkuu Mizengo Pinda, wajiuzulu kwa kushindwa kusimamia vizuri Operesheni Tokomeza Ujangili na kutatua migogoro ya wafugaji, wamegoma.

Tunasema kuwa mawaziri hawa wasingoje matokeo ya Tume ya Bunge, wapime wenyewe. Wakiona wanalazimika kubeba wajibu, wafanye hivyo.

Hii ndiyo tabia ya uadilifu kwa kiongozi.

Wednesday, October 30, 2013

Mbowe ataka wahamiaji haramu walipwe fidia

Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe
Na Debora Sanja, Dodoma:
KIONGOZI wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe (Chadema), ametaka wahamiaji haramu walioondoshwa nchini kwa kufanyiwa vitendo vya ukiukwaji wa haki za binadamu walipwe fidia.

Akiuliza swali la nyongeza bungeni jana, Mbowe alisema zoezi la Operesheni Kimbunga halikuwa na maandalizi ya kutosha na lilifanyika kwa chuki na uonevu.

“Waliokuwa wanafanya zoezi hili hawakujali mali za wananchi, hawakuangalia mazingira yaliyosababisha mtu kuwepo nchini na uchunguzi wa kutosha haukufanyika,” alisema.

Akijibu swali hilo, Waziri wa Nchi na Jeshi la Kujenga Taifa, Shamsi Vuai Nahodha alisema zoezi hilo la kuwaondoa wahamiaji haramu lilikuwa na nia njema.

Alisema ni kweli yapo malalamiko ya jinsi zoezi hilo lilivyokuwa linatekelezwa na kwamba Serikali itafanya kila linalowezekana kulichunguza jambo hilo.

Alisema ikibainika utaratibu wa kuwaondoa wahamiaji hao ulikiukwa, sheria zitachukuliwa kwa mujibu wa sheria.